MIAKA 30 YA TRA: TEKNOLOJIA NA HUDUMA BORA ZAIMARISHA UHUSIANO NA WALIPA KODI MKOA WA PWANI
Na Charles Kusaga, Pwani
Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) katika maadhimisho ya miaka 30 tangu kuanzishwa kwake tarehe 01 Julai 1996, imedhihirisha ukuaji wa huduma bora na teknolojia huku ikijivunia hatua kubwa iliyofikiwa katika kuimarisha mahusiano mema na ushirikiano thabiti na walipa kodi mkoa wa Pwani.
Akizungumza na wadau mbalimbali wa kodi mkoani hapa katika ufunguzi wa kongamano la maadhimisho ya miaka 30 ya TRA kwa mkoa wa Pwani Menejea wa Mamlaka ya Mapato Tanzania TRA Ndugu Peter Eliona alizungumzia mafanikio ya Mamlaka ya Mapato nchini.
Kwa mkoa wa Pwani alieleza kuwa katika kipindi hiki cha miongo mitatu, TRA Mkoa wa Pwani imeshuhudia mabadiliko makubwa kutoka katika mifumo ya kizamani ya ukusanyaji mapato na kuingia katika ulimwengu wa kidigitali. Mabadiliko haya ya kiteknolojia yamekuwa nguzo kuu katika kurahisisha utoaji wa huduma na kuondoa urasimu uliokuwa ukiwapa changamoto wafanyabiashara na wananchi mkoani humo.
Pia huduma bora, Elimu kwa wateja na ushirikiano mzuri kati ya Mamlaka na Walipa kodi kumeleta mafanikio makubwa ya ukusanyaji kodi. Uhusiano mzuri uliojengwa mkoani Pwani ndio siri ya mafanikio na ukuaji wa uchumi.
Miongoni mwa mambo yaliyochangia kwa kiasi kikubwa kuongezeka kwa mahusiano haya mazuri ni pamoja na:
Ukuaji wa Teknolojia na Mifumo ya Kidijitali: Kuanzishwa kwa mifumo ya kisasa ya kielektroniki (IDRAS) kumemwezesha mlipa kodi kupata huduma mahali popote alipo bila kulazimika kufika ofisi za TRA. Kazi kama vile kukadiria kodi, kuwasilisha ritani, kupata risiti (EFD) na kufanya malipo sasa zinamalizika kwa urahisi kupitia simu ya mkononi au kompyuta.
Kusogeza Huduma Karibu na Wananchi:
TRA Pwani imepanua wigo wake kwa kufungua vituo vya huduma na madawati ya ushauri katika wilaya na maeneo mbalimbali ya kimkakati mkoani Pwani ili kuhakikisha elimu ya kodi inamfikia kila mwananchi.
Kongamano hilo la maadhimisho lilifanikiwa kwa wadau mbalimbali wa kodi kutoa maoni yao na rai mbalimbali katika kutaua changamoto zilizopo kutoka kwa wananchi walipa kodi ili kuendelea kudumisha uhusiano huu mzuri uliopo.



Comments
Post a Comment