WAZIRI JAFO ASEMA HAKUNA HAJA YA KUFUATA BIDHAA KUTOKA NJE
Na Gustaphu Haule,Pwani
WAZIRI wa Viwanda na Biashara Dkt. Selemani Jafo ameeleza kuwa ndani ya muda mfupi ujao hakutakuwa na haja ya kuagiza bidhaa kutoka nje ya nchi kwakuwa Tanzania imejiimarisha katika kuzalisha bidhaa zake.
Jafo amesema kuwa kwasasa Tanzania inazalisha Bati,Vioo,Nondo,Saruji,TV ,simu na bidhaa nyingine na kwamba kutokana na hali hiyo hakuna haja ya kufuata bidhaa hizo nje kwakuwa Tanzania inazalisha bidhaa hizo na zenye viwango vya juu.
Jafo amebainisha hayo wakati wa ziara ya Rais Samia Julai 31,2025 mkoani Pwani ambapo alikuwa anafanya uzinduzi wa kongani ya Viwanda Kwala sambamba na uzinduzi wa bandari kavu ya kwala.
Waziri wa Viwanda na Biashara Selemani Jafo akisalimiana na Rais Dkt . Samia Suluhu Hassan wakati alipofanya ziara katika eneo la Kwala katika hafla ya kupokea Mabehewa mapya ya mizigo na uzinduzi wa Bandari Kavu ya Kwala leo Julai 31,2025.
"Ndani ya muda mfupi kuanzia sasa hakutakuwa na haja ya kuagiza bidhaa tena kutoka nje kwa mfano, mahitaji ya mabati kwa mwaka ni tani laki moja na elfu thelathini, leo hii makampuni yote yanayozalisha bidhaa hiyo ikiwamo ya Lodhia, king Lion,Alaf na imeweza kufikia tani laki 260,000 inamaana tunaakiba ya tani 130,000.
Aidha, ameeleza kwa lengo la kutaka kupunguza uingizaji wa bidhaa na kuongeza usafirishaji kuwa Wizara ya Viwanda na Biashara, itasimamia maono ya Rais Samia kuhakikisha Tanzania inakuwa nchi kinara kwa uzalishaji wa bidhaa, kusafirisha nje ya nchi na kuingiza fedha za kigeni.
Waziri wa Viwanda na Biashara Selemani Jafo wa kwanza Kulia akiwa katika picha ya pamoja na Rais Dkt .Samia Suluhu Hassan katika uzinduzi wa Kongani ya viwanda iliyofanyika Julai 31,2025 .
"Eneo la viwanda kwala lenye zaidi ya hekta 1000 zaidi ya viwanda 200 vitajengwa ambavyo uwekezaji wake ni zaidi ya dola za kimarekani bilioni tatu ambayo kwa mwaka mauzo yatakayopatikana kwa bidhaa zitakazozalishwa ni takribani Sh.bilioni 6 ambapo kati ya hizo Sh.bilioni 2 kwa usambazaji na bilioni 4 kwajili ya matumizi ya ndani.
Hatahivyo,Jafo amemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa anayoifanya na kwamba mafanikio ya ukuaji wa Viwanda nchini yanatokana na juhudi zake.
Mwisho
Comments
Post a Comment