WANANCHI 14,428 WAFIKIWA KAMPENI YA KISHERIA YA MAMA SAMIA KIBAHA VIJIJINI.
Na Gustaphu Haule,Pwani
Wataalam wa Kampeni ya msaada wa kisheria ya Mama Samia ( Mama Samia Legal Aid Campaign) wakiwa katika ofisi ya Katibu Tawala Wilaya ya Kibaha kwa ajili ya kukabidhi ripoti mara baada ya kumaliza kazi hiyo Machi 5, mwaka huu.
KAMPENI ya msaada wa Kisheria ya Mama Samia (Mama Samia Legal Aid Campaign) katika Halmashauri ya Wilaya ya Kibaha Mkoani Pwani imefanikiwa kuwafikia zaidi ya Wananchi 14,428.
Wakili wa Halmashauri ya Wilaya ya Kibaha Yasmin Makanya, ametoa taarifa hiyo Machi 6,2025 wakati akiwa katika kikao maalum na Katibu Tawala wa Wilaya ya Kibaha Moses Magogwa ikiwa sehemu ya kukabidhi ripoti ya kampeni hiyo.
Wakili wa Serikali katika Halmashauri ya Wilaya Kibaha Yasmin Makanya katika kikao cha kukabidhi ripoti ya kampeni ya Mama Samia (Mama Samia Legal Aid Campaign)
Aidha, Makanya katika kikao hicho ameongozana na baadhi ya timu iliyofanyakazi katika Halmashauri hiyo akiwemo afisa ardhi wa Halmashauri hiyo Neema Adrian,afisa maendeleo ya Jamii ambaye pia Msaidizi wa dawati la kisheria Diana Brandus na Mkuu wa dawati la Jinsia kutoka Wilaya ya Kipolisi Mlandizi Inspekta Tumaini Ulimboka.
Afisa Maendeleo ya Jamii na Msajili Msaidizi wa dawati la kisheria katika Halmashauri ya Wilaya Kibaha Diana Brandus (Kushoto)akimkabidhi ripoti ya Kampeni ya msaada wa kisheria Katibu Tawala Wilaya ya Kibaha Moses Magogwa hafla iliyofanyika Machi 6,2025 ofisini kwake.
Katika kikao hicho Makanya, amesema kuwa kampeni hiyo imefanyika katika Vijiji na Vitongoji 30 na kuwafikia Wananchi 14,428 ambapo kati ya hao Wanaume ni 7,410 na Wanawake ni 7,018.
Makanya , amesema pia katika kampeni hiyo wamefanikiwa kupokea migogoro 51 ambapo kati ya hiyo migogoro 18 imetatuliwa papo hapo huku migogoro 33 imekabidhiwa utawala kwa ajili ya kufanyiwa kazi.
Katika ripoti hiyo, Makanya amesema timu hiyo imebaini kuwa migogoro mingi inahusisha ardhi ikiwemo kugombea mipaka baina ya Kijiji cha Halmashauri Moja na Kijiji cha Halmashauri nyingine,wakulima na wafugaji,Wananchi na Wawekezaji na hata mwananchi kwa mwananchi.
Makanya, amesema kuwa pamoja na mafanikio hayo lakini timu hiyo imebaini kuwepo kwa changamoto ya miundombinu hususani ya barabara hali inayosababisha Wananchi kushindwa kufuatilia haki zao kwakuwa Vyombo vya Sheria vipo mbali nao.
Amesema, timu imeshauri kuona na namna ya kuendeleza kampeni hiyo ili kuongea elimu zaidi kwa Wananchi kwakuwa siku zilizowekwa ni chache lakini mahitaji yake ni makubwa .
"Utakuwa mtu mwingine ana makaratasi mengi (documents) lakini hajui wapi pa kuanzia katika kupata haki yake hivyo kuna kila sababu ya kampeni hii kupewaa kipaumbele na ikiwezekana iendelee kufanyika kwa maslahi ya Taifa na Wananchi wake,"amesema Makanya
Makanya ,amesema mbali na hilo lakini wameshauri kama inawezekana kusogeza Vyombo vya haki kwa Wananchi kwakuwa wengi wao wanashindwa kumudu gharama za za usafiri kwa ajili ya kufuata huduma za kisheria zilizopo Mijini.
Kwa upande wake Katibu Tawala Wilaya ya Kibaha Moses Magogwa, amemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt.Samia Suluhu Hassan kwa kuona umuhimu wa kufanya kampeni hiyo muhimu.
Katibu Tawala Wilaya ya Kibaha Moses Magogwa akizungumza na timu ya wataalam wa Kampeni ya msaada wa kisheria ya Mama Samia mara baada ya kupokea ripoti hiyo Machi 6,2025 kutoka katika timu hiyo.
Magogwa, amesema kampeni hiyo ni muhimu kwani imeonyesha Serikali ifanye nini kwa Wananchi wake lakini pia imekuwa sehemu ya msaada kwa Wananchi kwakuwa wengi wao shida zao zimetatuliwa.
Magogwa, amewapongeza wataalam wote wa kisheria pamoja na timu nzima iliyofanyakazi Wilaya ya Kibaha kwakuwa wameonyesha uzalendo wa kuwatumia Wananchi kwa moyo.
Amesema kuwa, kwa mujibu wa ripoti hiyo kazi nyingi zimefanyika na zingine zipo katika ufuatiliaji hususani jambo la mikapa na anafahamu kuna mambo yanatakiwa kufanyika ikiwemo suala la GN.
Amesema kuwa, kipaumbele cha Wilaya ni kuhakikisha Kibaha inapimwa na kupangwa lakini kwasasa zipo kliniki zinaendelea na kwamba kazi kuwa ni kutoa elimu na kusuluhisha masuala ya ardhi.
Magogwa, ametoa wito kwa Wananchi wanaotaka kununua ardhi wahakikishe wanakwenda katika ofisi za mkurugenzi wa Halmashauri hiyo ili kuondoa usumbufu wa kununua maeneo ambayo sio rasmi.
Hatahivyo, Magogwa amesema kuwa katika ofsi yake Kuna timu ya utatuzi wa migogoro ya ardhi ambayo hufanyika kila siku ya Jumatano .
Comments
Post a Comment