CHUO CHA MAENDELEO KIBAHA (FDC) CHAOMBEWA RUZUKU SERIKALINI
Julieth Ngarabali. Kibaha.
Chuo cha Maendeleo ya wananchi Kibaha (FDC) kinakabiliwa na changamoto mbalimbali na kupelekea Uongozi wa eneo hilo kuiomba Serikali isaidie fedha za ruzuku kwa ajili ya chakula na uendeshaji kama ilivyokuwa kwa vyuo vingine vya FDC vilivyopo chini ya Wizara ya Elimu.
Mkuu wa Chuo cha Maendeleo ya wananchi Kibaha Joseph Nchimbi pia ameiomba Serikali katika kipindi hiki ambapo kuna mabadiliko ya mitaa na kuweka mkazo kwenye mafunzo ya Amali itumie wataalamu katika chuo hicho na vyuo vingine kama hicho ambavyo tayari wana uzoefu katika kutoa mafunzo hayo ya Amali kwa kuwapanga wanafunzi wanaomaliza darasa la saba moja kwa moja kwenda kusoma fani mbalimbali za ujuzi.
Nchimbi ametoa maombi hayo Novemba 21 mjini Kibaha wakati akitoa taarifa ya chuo hicho kwa wananchi wa Kibaha, uongozi wa chuo na wa shirika la elimu Kibaha waliohudhuria kwenye mahafali ya 52 ya chuo ya chuo cha maendeleo ya wananchi Kibaha (FDC) ambapo vijana 147 wamehitimu mafunzo ya kozi ndefu ya miaka miwili katika fani mbalimbali za ujuzi ikiwemo ufundi bomba, umeme wa majumbani, ufundi magari, mifugo, uungaji na uundaji vyuma uchomeleaji ,upishi,ushonaji na kilimo.
Wahitimu wa Chuo cha Maendeleo ya Jamii Kibaha
Changamoto ingine aliyoitaja na kuomba Serikali isaidie ni pamoja na gari itakayorahisisha usafiri na usafirishaji chuoni, wameomba kupatiwa watumishi wanaohitajika ikiwemo wa fani za umeme, bomba na magari ili kumudu kutoa mafunzo ipasavyo na wameomba Serikali kuendelea kuwapatia fedha za kufanya ukarabati na kuongeza majengo mapya yanayohitajika na pia hawana karakana kwa fani za magari,umeme, useremala, ujenzi na bomba.
Awali Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Elimu Kibaha Robert Shilingi amesema mafunzo yanayotolewa chuo cha maendeleo ya wananchi Kibaha yanalenga kumpatia mwanachuo ufundi stadi unaomuwezesha kupambana na mazingira yake na kutokana na soko la ajira wanachuo hao hufanya mitihani ya VETA ili kujipima uelewa wao na kupata vyeti vinavyowawezesha kujiajiri au kupata ajira maeneo mbalimbali
Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Elimu Kibaha Robert Shilingi
Mkurugenzi wa Elimu, Ofisi ya Rais TAMISEMI Dokta Emmanuel Shindika akizungumza na wanachuo ,wazazi, viongozi wa shirika la elimu Kibaha pamoja na walimu wa chuo hicho amesema Serikali inatambua mchango wa vyuo vya mandeleo ya wananchi nchini na imeendelea kuboresha vyuo hivyo ikiwemo hicho cha Kibaha ambapo katika mwaka wa fedha 2022/2023 ilitoa sh. Milioni mia nne (400,000,000) ya ukarabati wa miundombinu kazi ambayo ameiona tayari imefanyika vema.
Mkurugenzi wa Elimu, Ofisi ya Rais TAMISEMI Dokta Emmanuel Shindika
Dkt. Shindika ameongeza kuwa Serikali inajipanga kuendelea kuleta fedha zingine za ukarabati wa mabweni ya wanachuo na miundombinu mingine hapo chuoni
“ napenda niwahakikishie wadau wa elimu nchini kuwa tutaendelea kushirikiana katika kuboresha mazingira ya kutoa mafunzo kwa kutenga bajeti kwa awamu hususan suala la miundombinu ,ukarabati na ujenzi wa majengo mapya ili kuleta ufanisi zaidi katika utoaji mafunzo yaliyobora”Amesema.
Aidha amewataka wahitimu kutumia ujuzi na maarifa waliyoyapata chuoni hapo katika kujenga a kuendeleza maisha yao pamoja na Taifa na kwamba njia rahisi ya kufanikiwa katika maisha ni kujiunga na vikundi vya uzalishaji mali kani watapata fursa ya kuunganisha nguvu ,ujuzi na kutumia rasilimali zitakazopatikana katika maeneo yao.


Comments
Post a Comment