WATOTO WATAJA VIBANDA UMIZA NA KAMALI VYANZO VYA UKATILI PWANI




Na. Julieth Ngarabali.

Utitiri wa vibanda vya maonyesho ya video na michezo ya kamali(kubeti) maeneo mbalimbali Mkoani Pwani kumeelezwa  kuwa ni baadhi ya vyanzo vinavyosababisha  kuenea vitendo vya ukatili na unyanyaswaji  dhidi ya watoto.

Mbali na maeneo hayo pia baadhi ya waendesha bodaboda wametajwa na watoto kuwa wamekuwa wakichangia wanafunzi kukatisha masomo kwa kuwapa ujauzito .

Hayo yamebainishwa baadhi ya wanafunzi kutoka shule za msingi na sekondari  za Halmashauri ya mji wa Kibaha Mkoani humo  kwenye mdahalo  uliokuwa na lengo la kujadili masuala mbalimbali  ikiwemo ya ukatili yanayowakabili watoto kuanzia umri wa miaka sefuri  na kuendelea ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya siku ya mtoto wa Afrika Mkoani humo

Katika mdahalo huo uliowashirikisha wadau mbalimbali wanaojihusisha na masuala ya watoto mada kuu tatu za ushiriki wa wadau katika kutokomeza ukatili wa jinsia ,wajibu wa wazazi na walezi katika kuwasaidia watoto kuzingatia maadili na ya tatu ni kuwasaidia na kuwapa watoto fursa za ujifunzaji naa stadi za kazi ziliwasilishwa na kujadiliwa .

Baadhi ya wanafunzi walioshiriki kwenye mdahalo wa kujadili masuala mbalimbali  ikiwemo ya ukatili na unyanyasaji.



"Watoto wengine hushindwa kumaliza darasa la saba na sekondari kutokana na mimba za utotoni zinazosababishwa na vishawishi hasa kwa waendesha bodaboda na ngoma zinazoandaliwa na familia"amesema Evelini Mhema wa shule ya msingi Miembe saba. 


Kutokana na hali hiyo amesema Seriikali inapaswa kuongeza kanuni ndani ya sheria zilizopo hasa kuwabana watu wanajiweka kando pindi wanapohitajika kutoa ushahidi mahakamani kwani wanasababisha kesi kukosa nguvu na watuhumiwa kuachiwa huru, 

"Serikali iweke kanuni za kuwabana wanajamii ambao kwa makusudi wamekuwa wakikwepa kwenda kutoa ushaihidi mahakamani pindi wanapoitwa kwani kuna baadhi ya wanajamii wamekuwa wakifanya hivyo huenda kwa maslahi binafsi"amesema

Aidha Mwanafunzi Johnson Alex amesema njia nyingine inayoweza kuwajenga watoto wasijiingize kwenye maeneo hatarishi ambayo yanawasababishia kutumbukia katika vitendo vya ukatili na unyanyaswaji ni viongozi wa dini kuendesha mihadhara yenye maudhui ya neno la Mungu. 

"Wapo baadhi ya watoto hasa wakike wamekuwa wakijirahisisha kwa madereva bodaboda kwa kuomba lifti na hada pesa za chipsi mwisho wa siku wanajikuta wanabakwa na haohao bodaboda kisha wanapata ujauzito hivyo kama watakuwa wanapewa mafundisho ya dini inaweza kusaidia"amesema

Wadau wa mdahalo wa kujadili masuala mbalimbali ya watoto  ikiwemo vitendo vya ukatili wakifatilia mada mbalimbali zilizokuwa zikiwasilishwa.

Mkurugenzi wa Yombayomba foundation inayojihusisha na kupinga ukatili Mjini Kibaha Altor Yombayomba  ametaja baadhi ya vitendo vinavyosababisha kuenea kwa vitendo vya ukatili dhidi ya watoto ni kucheleweshwa kwa mashauri pindi yanalofikishwa mahakamani huku zikitolewa sababu ambazo hazileti uzito.
 

"Utakuta kesi inapelekwa mahakamani baada ya hapo mizunguko inaanza mara upelelezi haujakamilika na siku zinakuwa zinaenda na baadaye shauri linakosa nguvu hivyo ni vema serikali ikaliangalia hilo ili kukomesha vitendo hivyo"amesema.

 Mkuu wa dawati la jinsia na watoto Mkoa wa Pwani kutoka Jeshi la Polisi  Eliezer Hokororo amesema jeshi hilo limejipanga kudhibiti vitendo vya ukatili dhidi ya watoto na wanachoomba ni kupata taarifa kwa wakati kutoka kwa wanajamii na kujotokeza kutoa ushahidi.

 Mgeni rasmi kwenye maadhimisho hayo Katibu Tawala msaidizi uchumi na uzalishaji Mkoa wa Pwani Shangwe Twamala amesema katika kudhibiti vitendo vya ukatili na unyanyaswaji dhidi ya watoto mkoa huo umekuwa ukitumia njia mbalimbali ikiwemo kutoa elimu na ulinzi na kwamba itaendelea kuongeza nguvu kwa kushirikuana na Taasisi mbalimbali

Mdahalo huo Juni 20 /2024  ulienda sambamba  na maadhimisho ya siku ya mtoto wa Afrika mkoani Pwani ambapo mgeni rasmi alikua Katibu Tawala msaidizi uchumi na uzalishaji Mkoa wa Pwani Shangwe Twamala   (katikati waliokaa)

Amewataka watoto kutokaa kimya pale wanapofanyiwa vitendo vya ukatili na bdala yake watoe taarifa ili wahusika waweze kuchukuliwa hatua kwa mujibu wa sheria za nchi na pia iwe fundisho kwa wengine ambao wanatabia hizo.

 

Mwisho










Club News Editor - Charles Kusaga

Comments

Popular posts from this blog

RC PWANI AONGOZA WAKAZI PWANI KUJIANDIKISHA KWENYE DAFTARI LA WAPIGA KURA

BARAZA LA MADIWANI KIBAHA MJINI LAMPONGEZA MKURUGENZI WAKE KWA KAZI NZURI ANAYOIFANYA SAMBAMBA NA KUONGEZA MAPATO.

RAIS SAMIA ATANGAZA KIBAHA MJINI KUWA MANISAPAA,MBUNGE KOKA AFURAHIA ASEMA KIBAHA ITANG'AA