Fahamu umuhimu wa wadudu katika Hifadhi ya Milima ya Udzungwa
Na Julieth Mkireri,Ifakara
Kwa takribani miaka 13 ilikuwa jambo la kawaida kwa wakazi wa Mangula B ikiwemo Bibiana Philipo (51) kwenda kuokota kuni katika hifadhi ya Udzungwa.
Anasema wamekuwa wakifanya hivyo katika Hifadhi ya milima ya Udzungwa ambayo ipo katika ushoroba wa Selou Udzungwa kuanzia mwaka 1987 hadi 2000 liipotokea katazo la kuingia katika hifadhi hiyo.
“Kuni tulizokuwa tunaokota baadhi zilikuwa zimeoza nilikuwa nikipasua kwa maandalizi ya kupikia nakutana na wadudu wenye rangi ya kijivu, hawa walikuwa bado hai wanatoka na kuanza kukimbia wakijihami wakati huo sikujua kama tunachofanya kina madhara kwenye uhifadhi,” anasema.
Katazo hilo la kuto okota kuni katika hifadhi ya Udzungwa ilikuwa ni njia bora ya kusaidia kulinda hifadhi hiyo pamoja na kuvutia utalii, hasa wanao fanya utalii wakutembea kwa kwa miguu kwa ajiikuona wadudu kama vipepeo, mende, na wadudu wengi.
Msomaji hifadhi ya Taifa ya Udzungwa ni mahali pazuri pa kutazama wadudu kwa sababu ya utofauti wake wa kipekee wa viumbe hai, hifadhi hii ina aina 5,000 za vipepeo, aina 800 za mende, na aina nyingi za wadudu wengine. Katika hifadhi hiyo mathalani kuna kipepeo mfalme, kipepeo blue morpho ambaye anajulikana kwa mabawa yake makubwa ya bluu


Mhifadhi wa Hifadhi ya Taifa ya Udzungwa Kamishna Msaidizi Abel Mtui anaeleza kuwa hifadhi hiyo ina wadudu wengi na kwamba kuna uwezekano wa asilimia 70 ya wadudu bado hawajatambuliwa.
Anataja baadhi ya wadudu waliopo kwenye hifadhi hiyo kuwa ni pamoja na jongoo, donbitoz, vipepeo aina ya milped na siafu ambao mtindo wa kutembea wakiwalinda malikia wao umekuwa kivutio kikubwa kwa watalii.
“Imebainika hivi karibuni kuanzia miaka ya 2001-2003 kuna wadudu aina ya jongoo wanapatikana hapa hifadhini pekee, kundi hili la wadudu ni lenye kazi kubwa lakini pia kivutio cha watalii na ni rasilimali kubwa ya kurutubisha ardhi,”anaeleza..


Jongoo ni aina ya wadudu wanaopatikana katika hifadhi ya Milima ya Udzungwa ambao ni moja ya vivutio na wana umuhimu mkubwa kama rasilimali ya kurutubishwa ardhi
Kamishna Mtui anasema hifadhi hiyo ya Udizungwa inaweza kuongoza kwa kuwa na aina nyingi za wadudu kuliko hifadhi nyingine kama ambavyo ilivyojizoela na umarufu mkubwa kwa ndege aina ya kwale.
Hali ya uharibifu wa mazingira inavyoathiri wadudu
Akizungumzia kuhusiana na uharibifu wa mazingira namna unavyosababisha wadudu kuondoka kwenye eneo lake Kamishna Mtui anasema, mwaka 2006 alishiriki kufanya utafiti wa maeneo ambayo yanaokotwa kuni kwenye hifadhi na ambayo hakuna shughuli kama hizo na kubaini kuwa na utofauti.
Anasema, katika utafiti huo walibaini maeneo yanayofikiwa na binadamu wakiokota kuni na magogo baadhi ya wadudu huondoka na wengine wanapata hofu na hivyo kushindwa kuendelea kuishi katika maeneo hayo tofauti na yale ambayo hayafikiwi na wadudu wengi wameendelea kuwepo.
Kamishna Mtui anasema katika maeneo ambayo shughuli za uokotaji kuni hazifanyiki wadudu wamekuwa wakiendelea kuzaliana huku mazingira yake yakiwa mazuri tofauti na sehemu ambazo kuni zinaokotwa mara kwa mara.
Kadhalika amesema walibaini katika maeneo hayo ambayo shughuli za kuokota kuni zinafanyika kuwepo na athari za kuwapo kwa mitego ya kunasia wanyama
“Maeneo hayo ambayo pia ni njia za watalii ilikuwa inaleta usumbufu na kuna wakati idadi ilipungua ikaonekana kuwa tunakiuka sheria za uhifadhi na kuanzia kipindi hicho ikaanzishwa miradi ambayo ililenga kutoa elimu kwa wananchi kuachana na tabia ya kuingia hifadhini na kuharibu shoroba,” anaeleza.
Nini kilifanywa kuondoa athari kama hizo
Kamishna Mtui anasema ushoroba anaoufanyia kazi ni ule unaounganisha Hifadhi ya Milima ya Udzungwa na Hifadhi ya Taifa ya Mwalimu Nyerere ambao una urefu wa kilomita za mraba 13 na unatoka kwenye hifadhi ya milima ya Udzungwa kwenda hifadhi ya Mwalimu Nyerere kupitia misitu wa asili wa Magombera.
Anasema ushoroba huo unafadhiliwa na Shirika lisilo la Kiserikali la Southern Tanzania Elephant Program (STEP) na kwamba maeneo yaliyo ainishwa ni mapito ya tembo mashamba na makazi ya wananchi yalifanyiwa uthamini na fidia na kulipwa ni katika Kijiji cha Sole,Mang’ula A na Kanyenja.
Ili kuondokana na uharibifu wa mazingira kwenye shoroba ya Selous Udzungwa anasema jitihada za kugawa miche ya miti kwa jamii na taasisi zilifanyika ili waachane na kuingia hifadhini kukata na kuokota kuni kwa ajili ya matumizi ya kupikia.
Kamishna Mtui anasema kasi ya wananchi kuingia msituni imepungua ukilinganisha na kipindi cha miaka mitano iliyopita na hiyo ni kutokana na elimu waliyopewa kuhusiana na utunzaji wa mazingira na madhara ya kufanya shughuli za kibinadamu kwenye misitu.
Pia mradi wa kuwezesha wananchi kimasomo na kipato ambapo mwananchi anapokuwa na kipato badala ya kutumia kuni atanunua gesi na kwa kufanya hivyo matumizi ya kuni yatapungua na hakutakuwa na uharibifu wa mazingira.
Makala hii imeandaliwa wakati wa mafunzo ya kuwajengewa uwezo waandishi wa habari namna ya kuandika habari za Bioanuai yaliyoratibiwa na kampuni ya Nukta Africa chini ya mradi wa USAID Tuhifadhi Maliasili.

Comments
Post a Comment