Serikali yapanua likizo ya Uzazi kwa wanaojifungua Njiti



Julieth Ngarabali, Pwani

Serikali imetangaza kupanua kipindi cha likizo ya uzazi kinachotambuliwa kisheria kwa wanawake katika utumishi wa umma wanaojifungua watoto wanaozaliwa kabla ya muda wake  maarufu njiti na kwamba hatua hii imepokelewa kwa mikono miwili na wadau mbalimbali ambao wamesema ni muhimu katika kuimarisha afya ya mama na mtoto.

Tangazo la Serikali la kupanua kipindi cha likizo ya uzazi kwa wanawake katika sekta ya umma wanaojifungua watoto njiti limekuja ikiwa ni mda mrefu sasa limekuwa likipigiwa kelele na wadau mbalimbali ikiwemo chama cha wafanyakazi wa Serikali kuu na afya (TUGHE) pamoja na wadau na masuala ya malezi, makuzi na maendeleo ya awali ya mtoto kupitia programu Jumuishi ya PJT-MMMAM ambao unalenga kutatua changamoto za ukuaji na maendeleo ya awali ya watoto wa umri wa miaka 0-8 

Akizungumza kwa niaba ya Rais Samia Suluhu Hassan wakati wa sherehe za siku ya Wafanyakazi mwaka 2024 Mkoani Arusha , Makamu wa Rais Philip Mpango amesema kuanzia sasa likizo ya wanawake wanaofanya kazi katika sekta ya umma itaanza mara tu watoto wanaozaliwa mapema yaani Njiti watakapotoka katika chumba cha uangalizi maalum.

Ameongeza kuwa wanawake wenye watoto njiti wanapaswa pia kupewa muda wa kunyonyesha kwa miezi sita ili kuhakikisha watoto wao hao wanapata uangalizi bora zaidi.

"Serikali imewekeza fedha nyingi katika huduma za afya ya mama na mtoto, ikiwa ni pamoja na kuanzisha vyumba zaidi vya uangalizi wa watoto njiti kwa hivyo naagiza kwamba likizo ya uzazi katika hali kama hizo ianze mtoto anapotoka katika chumba cha uangalizi maalum kama itakavyoamuliwa na madaktari." Amesema Dk. Mpango.

Picha ni Makamu wa Rais Dokta Philip Mpango.

Dk. Mpango amebainisha kuwa wafanyakazi wanaojifungua watoto njiti wamepewa ruhusa ya kuondoka kazini saa 07.30  kwa muda wa miezi sita baada ya kumaliza likizo yao ya uzazi ili kuwapa muda wa kutosha wa kunyonyesha.

Amebainisha kuwa kwa wafanyakazi wa sekta binafsi, Serikali pia itafanyia marekebisho sheria husika ili nao wanufaike, sheria hiyo ni sheria ya ajira na mahusiano kazini  sura ya 366 na marekebisho yake ya mwaka 2019 .

Uamuzi huo umepokelewa kwa mikono miwili na wadau wa masuala ya mama na mtoto nchini, wakisema umechelewa kuchukuliwa.

Kwa mujibu wa Shirika la Afya Duniani (WHO) mtoto anachukuliwa kuwa ni njiti ikiwa tu amezaliwa kabla ya wiki 37 za ujauzito.

Mkurugenzi Mtendaji wa Mtandao wa Programu za Jinsia Tanzania (TGNP) Lilian Liundi amesema uamuzi huo utasaidia kina mama kufanya malezi ya watoto hao ambao kimsingi ni wenye mahitaji maalum.

Ameongeza kuwa, hata hivyo, Serikali iongeze bajeti ya Wizara ya Afya ili kukidhi mahitaji ya vifaa vya kisasa vya kutunza watoto Njiti.

Kwa mujibu wa hotuba ya Waziri wa Afya Ummy Mwalimu Bungeni Dododom, kuhusu makisio ya mapato na matumizi ya fedha ya Wizara hiyo kwa mwaka 2023/2024 bajeti yake kwa kipindi hicho ni sh. Trilioni 1.235 ikiwa na ongezeko la sh. Bilioni 121 ukilinganisha na bajeti ya 2022/2023 sawa na ongezeko la asilimia 10.9 kuongezeka kwa bajeti hii kulilenga pia kuboresha huduma za afya kwa mama na mtoto nchini.

Nini anachokisema mmoja wa wanawake waliowahi kujifugua mtoto Njiti;

 Naye mmoja wa wanawake waliowahi kujifugua mtoto njiti ambaye pia ni mtumishi katika  Hospitali  ya rufaa ya mkoa wa Pwani yaTumbi  Felister Assenga amesema hatua hiyo isiishe katika hatua ya tangazo na kushaui kuwa mabadiliko hayo yanahitaji kupelekwa Bungeni ili yawe sehemu ya sheria ya kazi .

Picha ni mmoja wa wanawake waliowahi kujifugua mtoto njiti ambaye pia ni mtumishi katika  Hospitali  ya rufaa ya mkoa wa Pwani yaTumbi  Felister Assenga .

"Ni muhimu iingizwe katika sheria ya kazi na kurasmishwa ili hata waajiri waweze kuichukua na kuitekeleza katika ofisi zao  na pia tunaishukuru Serikali kwa hatua hii nzuri ya mwanzo’’amesema 

Mapema mwezi machi Mwaka huu 2024 ,Wafanya kazi  wanawake  waliojifungua watoto kabla ya muda  wake maarufu watoto  njiti  waljitokeza hadharani na kusema siku 84 zilizowekwa kisheria kama likizo ya uzazi hazitoshelezi  kulea  watoto njiti  na kwamba kuna umuhimu wa Serikali kuangalia upya  uwezekano wa kuboresha sheria ya ajira na mahusiano kazini  sura ya 366 na marekebisho yake ya mwaka 2019 .

Katika sheria hiyo kifungu kidogo cha 33 kifungu kidogo cha 6 (a ) kinasema mtumishi mwanamke aliyejifungua mtoto mmoja atapata likizo ya siku 84  huku kifungu cha 33 kifungu kidogo cha 6 ( b ) inaeleza kuwa mtumishi mwanamke aliyejifungua watoto zaidi ya mmoja atapata likizo ya siku 100 ambapo sheria hiyo imeishia hapo haijasema kama atajifungua watoto njiti atapata muda wa ziada na hivyo shida imeanzia hapo 

Chanzo cha kuzaliwa watoto njiti .

Kwa mujibu wa shirika la Afya Duniani (WHO) maradhi katika njia ya mkojo (UTI ) wanawake wenye historia ya kupatwa na uchungu mapemawapo katika hatari ya kujifungua njiti ukilinganisha na wasio na historia hiyo, kuwa na mimba yenye zaidi ya mtoto mmoja ,wanawake wenye matatizo katika maumbile ya mfumo wa uzazi nao wapo katika hatari zaidi, maradhi yanayosabishwa na ngono zembe ikiwemo Ukimwi,kisonono ,kaswende na trikomonasi.

Ingine ni shinikizo la damu ,kutokwa na damu katika sehemu za uzazi ,mama kuwa na uzito mdogo  au mkubwa kupitiliza wakati wa ujauzito,wanawake walio na umri unaozidi miaka 35 wapo katika hatari pia, msongo wa mawazo na matatizo ya kifamilia

Hali ikoje

Kwa mujibu shirika la Umoja wa Mataifa la afya Duniani WHO na shirika la umoja wa mataifa la kuhudumia watoto UNICEF makadirio yanaonyesha kwamba mwaka 2020 takribani watoto milioni 13.4 walizaliwa kabla ya muda yaani njiti huku karibu milioni 1 kati yao wakifariki kutokana na matatizo yanayotokana na hali hiyo ya kuzaliwa kabla ya wakati .

Aidha Afisa elimu kazi wa chama cha wafanyakazi wa Serikali kuu na afya (TUGHE) makao makuu Nsubisi  Mwasandende amesema  sheria ya sasa ya  ajira na mahusiano kazini imekuwa ikitoa siku 84 kwa wanawake wanaojifungua mtoto mmoja na siku 100 kwa wanaojifungua zaidi ya mtoto mmoja .

Lakini sheria hiyo haisemi chochote kuhusu wale wanawake wanaojifungua watoto njiti  na ndio maana walijitokeza hadharani kuikumbusha Serikali ifanyie kazi changamoto hiyo.

Afisa elimu kazi wa chama cha wafanyakazi wa Serikali kuu na afya (TUGHE) makao makuu Nsubisi  Mwasandende 

"Sheria ya sasa ya  ajira na mahusiano kazini imekuwa ikitoa siku 84 kwa wanawake wanaojifungua mtoto mmoja na pia siku 100 kwa wanaojifungua zaidi ya mtoto mmoja  wala haisemi chochote kuhusu wanawake wanaojifungua watoto njiti ndio maana tumeona ni vyema kuikumbusha Serikali ili ifanye mabadiliko ili kuwaongezea muda wanawake hao"amesema  Mwasandende

Matatizo kadhaa yanayoweza kumkumba mtoto njiti

Matatizo yanayowakumba zaidi watoto njiti ni pamoja na kupumua kwa sababu wakati huu mapafu yanakua hayajakomaa, shida ingine mi kwenye ulaji au unywaji kutokana na mfumo change wa chakula 

Aidha Programu Jumuishi ya Taifa ya malezi, makuzi na maendeleo ya awali ya mtoto (PJT-MMMAM ) tayari imeanza kutekelezwa nchini  na unalenga kutatua changamoto za ukuaji na maendeleo ya awali ya watoto wenye umri wa miaka 0-8 kupitia afua tano ikiwemo lishe ya kutosha kuanzia ujauzito, afya bora kwa mtoto na mama/mlezi ,malezi yenye muitikio ,fursa za ujifunzaji wa awali ,ulinzi na usalama kwa watoto.









Club News Editor - Charles Kusaga

Comments

Popular posts from this blog

RC PWANI AONGOZA WAKAZI PWANI KUJIANDIKISHA KWENYE DAFTARI LA WAPIGA KURA

BARAZA LA MADIWANI KIBAHA MJINI LAMPONGEZA MKURUGENZI WAKE KWA KAZI NZURI ANAYOIFANYA SAMBAMBA NA KUONGEZA MAPATO.

RAIS SAMIA ATANGAZA KIBAHA MJINI KUWA MANISAPAA,MBUNGE KOKA AFURAHIA ASEMA KIBAHA ITANG'AA