DAKTARI BINGWA WA SARATANI ATETA NA VIONGOZI WA DINI PWANI

Na Gustaphu Haule
MJUMBE wa kamati ya Siasa Mkoa wa Pwani Dr. Chakou Tindwa,amewashauri viongozi mbalimbali kuwa waadilifu ili kulinda amani iliyopo kwani kufanya hivyo itakuwa njia sahihi ya kumuenzi Rais Dkt.Samia Suluhu Hassan anayefanyakazi huku akiwaheshimu wananchi wake.
Tindwa ambaye pia ni daktari bingwa wa magonjwa ya saratani hapa nchini na mdau wa maendeleo anayesaidia masuala ya kijamii ametoa ushauri huo katika kongamano la Jumuiya ya Maridhiano na Amani Tanzania (JMAT)lililofanyika Februari 07 Wilayani Mkuranga.
Dr.Tindwa, amesema kuwa uadilifu mara nyingi unaambatana na kutii mamlaka iliyopo na kwamba bila kutii mamlaka ni Wazi kuwa hakuna uadilifu jambo ambalo linaweza kusababisha kuvunjika kwa amani.
Aidha,katika kongamano hilo ambalo Tindwa alikuwa mgeni rasmi amewasisitiza washiriki hao kuzingatia mambo makuu matatu ikiwemo kuwaheshimu na kuwahudumia wananchi wenye uhitaji ,kutenda haki kwa mamlaka ya mtu aliyonayo pamoja na kuheshimu mamlaka zilizopo.
"Ninyi viongozi wa dini ndio makamisaa wetu katika jamii kwasababu kuna makamisaa wa kimamlaka na kijamii ambapo makamisaa wetu katika jamii ndio viongozi wetu wa dini,"amesema Tindwa
Tindwa,amewaomba viongozi hao wa dini kama wakiona kuna changamoto wasisite kuzieleza na kuelekeza kwani uadilifu ni kichocheo cha kuleta amani na kwamba amani inapovunjika tunakuwa katika hatari.
Dr .Tindwa ambaye kiasili ni mwenyeji wa Kijiji cha Kibuyuni ,Kitongoji cha Kibwala Kata ya Panzuo Wilayani Mkuranga amewashauri viongozi hao wa dini kuandaa kongamano la amani ambalo litashirikisha madhehebu yote bila ubaguzi.
" Katika kuombeana amani na kumuunga mkono Rais Samia kwa kazi kubwa anayoifanya hususani kwa kuleta maendeleo na kudumisha Maridhiano ya amani kwa Taifa letu nawashauri viongozi wangu wa dini kuandaa kongamano lingine ambalo litajumuisha madhehebu yote bila ubaguzi ili kusudi tufanye maombi kwa pamoja,"amesema Tindwa
Mwenyekiti wa kongamano hilo Shukuru Ngweshani,amesema kuwa kongamano hilo limewashirikisha wadau mbalimbali wa masuala ya amani zikiwemo Taasisi za Serikali,vyombo vya utoaji haki Kwa wananchi vilivyopo Wilayani Mkuranga.
Club News Editor Julieth Ngarabali
Comments
Post a Comment