BAADHI YA ASASI CHANZO CHA KUKWAMISHA UFANISI WA PROGRAM YA MALEZI.MAKUZI NA MAENDELEO YA AWALI YA MTOTO



  •        Ni kwa kuwakwepa maafisa maendeleo ya jamii
  •       Baadhi zaanza kuchukuliwa hatua.
  • Serikali yaonya   

Julieth Ngarabali, Pwani.

Moja ya wadau wakubwa katika utekelezaji wa program jumuishi ya Taifa ya malezi,makuzi na maendeleo ya awali ya mtoto ni maafisa ustawi wa jamii ambao hufanya kazi kwa niaba ya Serikali katika kusimamia utekelezaji wa Pogram hii ambayo Serikali imetoa maelekezo ya utekelezaji wake kusambaa maeneo yote nchini ifikapo mwezi wa nne mwaka huu.

Katika mkutano wa mwaka uliofanyika mwezi Disemba mwaka 2023 na kuwakutanisha wadau wote kutoka Serikalini, asasi za kiraia pamoja na waandishi wa habari,msukumo mkubwa ulikuwa kutengeneza muunganiko wa pamoja kati ya wadau muhimun ili elimu juu ya malezi,makuzi na maendeleo ya awali ya mtoto kuanzia umri wa miaka 0-8 iweze kuifikia jamii na kuelewa huku kilio kikubwa kikitajwa kwa baadhi ya wadau kutoshiriki kikamilifu ama kukwepa kufuata taratibu kama zilivyoainishwa na mpango huu wa Taifa.

Mkoani Pwani baadhi ya asasi za kiraia zinazojihusisha na masuala ya malezi, makuzi na maendelo ya awali ya mtoto wakiwemo wa  umri chini ya miaka nane zimebainika kukwepa  kuwashirikisha Maafisa Maendeleo ya jamii kwenye shughuli zao wanazofanya katika jamii na hivyo kufanya mambo kinyume na maadili ya kitanzania na ya usajili wao. 

Uchunguzi uliofanywa na mwandishi,umebaini kuwepo kwa taasisi isiyo ya kiserikali katika moja ya kijiji Wilayani Bagamoyo mkoani Pwani ambayo inaendesha shughuli za kulea watoto wakiwemo wenye umri chini ya miaka 8 bila kufuata muongozo wa Taifa wa Program ya malezi,makuzi na maendeleo ya awali ya mtoto huku shughuli zake zikiendeshwa bila kuihusisha ofisi ya afisa maendeleo ya jamii Wilaya.

Asasi hiyo iliyotambulika kwa jina la Mango Kinder ambayo inatuhumiwa kutoa elimu isiyo na maadili ya ki Tanzania kwa watoto wadogo wakiwemo wa chini ya miaka nane katika kijiji cha Duda Bagamoyo ambapo toka Novemba 2023 ilikua ikiwakusanya watoto wengi kutoka maeneo mbalimbali Bagamoyo kwa madai ya kuwapa elimu ambayo  hata hivyo imetiliwa shaka.

" Februari 06 mwaka 2024 imegundulika kuwepo taasisi moja ya Mango Kinder ambayo inatuhumiwa kufanya malezi na kutoa elimu isiyo na maadili ya ki Tanzania kwa watoto wadogo wakiwemo wa chini ya miaka nane katika kijiji cha Duda Bagamoyon na hawa waliwakwepa maafisa maendeleo jamii wakawa wanajifanyia wanavyotaka,sio sahihi kabisa"' amesema Bi. Judith Mayunga,afisa maeneelo ya Jamii kata ya Dunda,Wilaya ya Bagamoyo Mkoa wa Pwani.

   Afisa maendeleo ya Jamii kata ya Dunda Wilayani Bagamoyo Mkoani Pwani  Judithi Mayunga .

Judithi ameeleza kuwepo kwa changamoto hiyo ya baadhi ya asasi za kiraia zinazojihusisha na masuala ya malezi ya watoto wakiwemo wa chini ya miaka nane kwenye uzinduzi wa Programu Jumuishi ya Taifa ya malezi, makuzi na maendeleo ya awali ya mtoto kwa Halmashauri ya Wilaya ya Bagamoyo mkoani Pwani mpango ambao unalenga kutatua changamoto za ukuaji na maendeleo ya watoto wenye umri wa miaka 0-8 .

 Ameongeza kuwa ni muhimu na ni lazima kwa asasi zote za kiraia zinazofaya kazi za watoto kushirikiana na maafisa hao ngazi ya kata kwa sababu wanachotaka kujua maafisa hao ni huduma zinazotolewa kama zinaendana na malezi,makuzi na maadili kwa mtoto pamoja na mazingira rafiki.

“Ikumbukwe kwamba malezi ni matendo yote yanayofanywa na wazazi, walezi na jamii ikiwemo asasi za kiraia zinazojihusisha na msuala hayo kwa lengo la kumlea ,kumkuza,kumlinda,kumuendeleza mtoto kimwili,kiakili ,kijamii,kihisia na kimaadili ili aweze kuishi ,kukua vizuri na kukubalika na jamii”. Amesema Judith

Katika misingi hiyo yapo mambo muhimu ambayo kila mmoja anapaswa kuyazingatia wakati wote wa malezi na makuzi , moja wapo ni afya hapa mtoto anahitaji kupatiwa tiba na kinga zote dhidi ya marathi ya kuambukiza kwa njia ya chanjo,lishe  kwa maana ya chakula bora ama lishe kamili,uchangamshi ,uangalizi kwa maana ya ulinzi wakati wote katika mazingira anayokuwepo mtoto  mamba ambayo yote haya asasi zinatakiwa kuweka wazi nini wanachokifanya lakini baadhi huwahofia maafisa hao.


Mkurugenzi wa taasisi ya ANJITA Janeth Christian akitoa mada ya malezi, makuzi na maendeleo ya awali  ya mtoto kwenye uzinduzi wa PJT-MMMAM Bagamoyo.

Kwa Upande wake Mkuu wa Wilaya hiyo Halima Okash alifika kituoni hapo na kuwakuta watoto zaidi ya 200 pamoja na zana mbalimbali ambazo imempelekea kugundua kuwa watoto hao wakiwemo wa chini ya miaka nane walikua hawafundishwi maadili mema na mengi ya mambo wanayofundishwa ni ya kijinsia ambayo yanakiuka taratibu,mila na desturi za Tanzania

Uamuzi wa Serikali ilikuwa ni kuisitishia kibali na leseni ya taasisi hiyo  na wote wanaohusika na taasisi hiyo huku wahusika wakichukuliwa kwa ajili ya mahojiano na uchunguzi zaidi. 

Katika uzinduzi huo wa PJT-MMMAM Bagamoyo taasisi hiyo imetajwa ni mojawapo ya zinazodaiwa kuwakwepa maafisa maendeleo ya jamii na hivyo  kutakiwa sasa kutoa ushirikiano kwani zikibainika zinakwenda kinyume na usajili wake zitachukuliwa hatua ikiwemo kufungiwa kama hiyo ya Mango Kinder.

“’Asasi za kiraia tunajua ninyi ni wadau wetu wakubwa wa maendeleo na malezi ya watoto wakiwemo hawa wa miaka chini ya nane mnafanya kazi zetu kwenye kata na sisi Maafisa maendeleo ya jamii ndio waratibu huko lakini mnatukwepa sijui mnadhani tutawaomba posho, kitu ambacho sio kweli msiwe na hofu hii, sisi tunachotaka kujua ni mnachofanya kama  kinaendana na maadili ya mtoto”amesema  Judithi.Baadhi ya wadau wa PJT - MMMAM  Bagamoyo.

Naye Mkuu wa Polisi Jamii Bagamoyo Fardina Hozza ameongeza kuwa katika kesi wanazopata inaonyesha wazazi na walezi wengi wamejitenga kulea watoto wao wameelekeza nguvu zaidi katika mambo mengine ya kijamii  na kiuchumi ambayo hayahusiani zaidi na malezi bora.

“Watu wanaondoka alfajiri watoto wamelala na wanarudi usiku wamelala ,wanaobaki wanakuwa bize na mambo yao tu hawazingatii chochote huku nyuma hajui mtoto amebaki na msichana wa kazi au mjomba wake au dada yake je analelewa vipi?’’ amehoji na kuongeza

“ Kwa hiyo watoto sasa hivi wanakua ilimradi tu kitu ambacho mbali ya kukosa maadili mema wanakutana na ukatili aina tofauti tofauti na wakiletwa kituoni unakuta ameshaharibiwa mbele na nyuma mda mrefu hata zaidi ya wiki sita” amesema Hozza.

Amesema Bagamoyo baada ya kutoa elimu na kuweka sheria thabiti  sasa kesi za ukatili za watoto zimepungua kwa kiasi kikubwa lakini mwanzo ilikua ni hatari unakuta mtoto wa miaka mitano, minne au miwili amebakwa na mjomba wake, kijana wa kazi au babu yake

“ Kwa hiyo sasa kupitia Programu hii ya PJT ‘MMMAM tukijumuika kwa pamoja kwa sababu sisi hua tunafanya dawati kama dawati  lakini tukiwa jumuishi tukafanya kazi pamoja tutaweza kufika mbali zaidi katika malezi, makuzi na maendeleo ya awali watoto hasa hawa chini ya miaka nane”’ amesema Hozza ambaye ni Mkuu wa Polisi Jamii Bagamoyo.

 Mganga Mkuu wa Hospitali ya Bagamoyo ameshauri wadau wa programu hiyo  kushirikiana na serikali katika kuratibu na kuomba Halmashauri itenge bajeti ya kufanikisha mpango huo.  

Shabani Omari ni mmoja wa wazazi wenye watoto waliokutwa kwenye taasisi hiyo iliyofungiwa anasema Serikali iwe inafanya ufuatiliaji wa kina kwenye vituo vinavyokusanya watoto chini ya miaka nane kwa sababu ndio inayowapa leseni ya kulea watoto ,kuliko kumlaumu mzazi ambaye yeye anachofahamu mtoto yupo kituo salama kwa sababu kimesajiliwa na Serikali na wapo maafisa ukaguzi wa elimu , ustawi wa jamii na mendeleo ya jamii.

Katika mkoa wa Pwani mpango huo wa PJT -MMMAM  inatekelezwa na taasisi ya ANJITA kwa kushirikiana na Serikali kwenye eneo la afya bora ,lishe ya kutosha kuanzia ujauzito, malezi yenye muitikio,fursa za ujifunzaji wa awali, ulinzi na usalama kwa watoto,

Mkoa wa Pwani, kupitia madawati ya ustawi wa Jamii na maeneo ya utoaji huduma za kijinsia katika Halmashauri yamepokea migogoro ya ndoa 689 ,matunzo 908 na migogoro inayohusu watoto wa nje ya ndoa 973 katika kipindi cha Julai hadi Disemba 2022 .











Club News Editor

Comments

Popular posts from this blog

RC PWANI AONGOZA WAKAZI PWANI KUJIANDIKISHA KWENYE DAFTARI LA WAPIGA KURA

BARAZA LA MADIWANI KIBAHA MJINI LAMPONGEZA MKURUGENZI WAKE KWA KAZI NZURI ANAYOIFANYA SAMBAMBA NA KUONGEZA MAPATO.

RAIS SAMIA ATANGAZA KIBAHA MJINI KUWA MANISAPAA,MBUNGE KOKA AFURAHIA ASEMA KIBAHA ITANG'AA