Chungu, tamu: Pori la Akiba la Kilombero kupandishwa hadhi
Na Monica Msomba.
Kilombero. Ni mwendo wa saa tano kutoka Halmashauri ya Mji wa Ifakara hadi kufika katika Pori la Akiba la Kilombero “A” lililopo Halmashauri ya Wilaya ya Mlimba mkoani Morogoro.
Nafika katika bwawa la Ndolo
lililopo katika pori hilo. Nakuta hali ya bwawa hilo ni tulivu huku sehemu
kubwa ikiwa imefunikwa na majani kana kwamba hakuna bwawa kabisa.
Hali iliyopo sasa hivi usingeweza kuikuta miezi 10 iliyopita. Bwawa hilo liligeuka kuwa shamba la bibi kwa wavuvi na wafugaji kuvua samaki na kunyeshwa mifugo yao.
Wangeachwa waendelee kuendesha
shughuli hizo ambazo ziko kinyume na sheria, huenda bwawa hilo lingetoweka
kabisa na viumbe hai vilivyokuwa vikiishi katika bwawa hilo navyo vingetoweka.
Sheria ya Uhifadhi ya Mamlaka ya
Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania (TAWA) namba 5 ya mwaka 2009 inaeleza kuwa
mtu yeyote anayekutwa katika hifadhi akifanya shughuli yoyote ya kibinadamu
akikamatwa atakuwa amefanya kosa la jinai.
Kwa sasa kila kitu kimebadilika.
Serikali iliingilia kati kuliokoa bwawa la Ndolo kwa kuweka utaratibu mpya wa
kutoa vibali vya uvuvi na kupiga marufuku wamiliki wa mifugo kuingiza mifugo
katika bwawa hilo.
Hatua hiyo ilikuja baada ya Pori la
Akiba la Kilombero lenye ukubwa wa kilomita za mraba 6,989.3 kupandishwa hadhi
kutoka Pori Tengefu la Kilombero Februari 17, 2023 kwa tangazo la serikali
namba 64.
Pori hilo linalopakana na Vijiji 92 limegawanyika katika sehemu mbili ‘A’ ambalo lina ukubwa wa kilomita za mraba 2,381.5 na zilizobaki ni Pori la Akiba Kilombero “B”
Mwelekeo mpya wa uvuvi
Mamlaka ya Wanyamapori Tanzania
Kilombero (TAWA) imeanza kutoa vibali kwa wananchi waishio jirani na pori hilo
hasa wanaojishughulisha na uvuvi katika mabwawa yaliyopo ndani ya pori hilo.
Lengo la utaratibu huo ni kupambana
na uvuvi haramu ili kulinda viumbe vya majini wakiwemo samaki wanaopatikana
katika mabwawa la Ndolo.
Afisa Ujirani Mwema wa Pori la Akiba
la Kilombero, Rehema Kaminyoge anasema wameweka miongozo ya namna ya kuvua
samaki ambapo sharti mojawapo ni kusajiliwa na kupata kibali kulingana na
mahitaji ya wavuvi.
Pia mvuvi anatakiwa kuwa na leseni
ya uvuvi kutoka halmashauri husika.
' Kasi ya wavuvi hao kukata vibali
bado ni ndogo kwani mpaka Novemba 30 mwaka huu walikuwa wamekata vibali wavuvi
nane lakini baada ya kuona hali hiyo kwa sasa tumeweka mpango wa kuhakikisha
tunawapeleka wataalamu pale kambini ili waweze kusaidiwa kirahisi"anasema
Rehema.
Wavuvi watoa ya
moyoni
Mmoja wa Wavuvi katika kambi ya
wavuvi ya Ishelelo, Kijiji cha Idui, Eliud Daniel (52) anaeleza furaha yake
kuhusiana na mpango wa kukata vibali uliowekwa na TAWA Kilombero kwani
utasaidia kulinda mazingira. Daniel ambaye ana mke na watoto watano ameishauri
Serikali kuangalia namna ya kupunguza gharama za kukata vibali angalau ifikie
Sh.4,000 kwani viwango vilivyowekwa kwa sasa wanashindwa kumudu.
Mwenyekiti wa Kijiji cha Idui, John
Laurent (54) anasema kuwa utaratibu uliowekwa ni mzuri na wako tayari
kuutekeleza kwa kuwa shughuli ya uvuvi ndio sehemu ya kipato ambacho kinasaidia
kuendesha maisha yao na hata kusomesha watoto wao.
‘’Utaratibu wa kukata vibali kwetu sisi ni mzuri kwa kuwa utasaidia wavuvi kufanya shughuli zetu tukiwa huru na hii itatusaidia kuwa na uvuvi endelevu na wenye tija ambao utatufanya tuwe na kipato cha uhakika na hivyo kuinua uchumi wa familia zetu.
“Tunaomba utaratibu wa kukata vibali uwekwe vizuri ili kuwarahisishia wavuvi kupata kibali kwa urahisi,” anasema Laurent.
Kwa upande wake,
mfanyabiashara wa samaki wa Kijiji cha Idui, Mwanaisha Katembo (43) anaiomba
TAWA Kilombero kuhakikisha wanaweka utaratibu mzuri ambao utawasaidia wavuvi kupata
vibali kwa urahisi na kuondoa usumbufu kwa wachuuzi.
Anasema kwa sasa mvuvi analazimika
kusafiri umbali wa kilomita 200 kutoka katika kijiji chao mpaka kufika katika
ofisi za TAWA zilizopo katika Halmashauri ya Mji wa Ifakara kwa ajili ya kukata
kibali.
Mwanaisha anadai jambo hilo limekuwa
likiwakatisha tamaa kwa kuwa gharama ya kusafiri ni kubwa kuliko hata ile ya
kukata kibali husika.
“Binafsi nimeridhishwa na utaratibu
wa wavuvi kukata vibali, utaleta manufaa kwa wafanyabiashara na hata wavuvi wenyewe
kwani hapo awali kulikuwa na uvuvi holela ambao ulisababisha wakati mwingine
bwawa kupungua maji na hata kukosa samaki. Uvuvi huo ulikuwa unaua mazalia ya
samaki,” anasema Mwanaisha, mchuuzi wa samaki .
Picha ni baadhi ya Wavuvi katika kambi ya wavuvi ya Ishelelo kijiji cha Idui Kilombero
Wadau waungana
kulinda bwawa Ndolo
Mwekezaji wa kampuni ya Kilombero
Safari, James Bebe anasema kuwa wanashirikiana na TAWA kufanya doria usiku na
mchana ili kuzidhibiti vitendo vya uharifu na shughuli nyingine za kibinadamu
ndani ya hifadhi.
Bebe anasema hali ya uvuvi kwa sasa
ni nzuri kwani wavuvi wanafuata utaratibu uliowekwa.
“Kuna sehemu tumezuia wavuvi wa
kiraia hawawezi kuingia hovyo lakini mkakati mkubwa uliopo ni kuongeza ulinzii
zaidi ili kuhakikisha hifadhi inakuwa salama na vitendo vya kiharifu
vinakomeshwa,” anasema Bebe na kuongeza
“Kampuni yetu imeingia mkataba wa
kushirikiana na TAWA kuhakikisha tunalinda na kutunza vivutio vyote vilivyopo
katika hifadhi hii, ndio maana tumeongeza nguvu ya ulinzi na sasa tunalinda
usiku na mchana na hata mimi mwenyewe ninashiriki ulinzi huu."
Bebe alikuwa akizungumza wakati wa mafunzo kwa vitendo ya kuripoti habari za bioanuai yaliyoandaliwa na kampuni ya Nukta Africa chini ya mradi wa USAID Tuhifadhi Maliasili.
Umuhimu wa bwawa Ndolo
Bwawa la Ndolo ni miongoni mwa
mabwawa matatu yaliyopo katika Pori la Akiba la Kilombero, Mabwawa mengine ni
Ngapemba na Mende.
Mabwawa hayo yamekuwa yakizalisha
samaki aina ya Vitoga, Kambale na samaki maarufu duniani aina ya “Tigerfish”
ambaye amekuwa kivutio kikubwa cha watalii kwa kuwa hupatikana zaidi katika
bwawa Ndolo.
Pia bwawa hilo ni muhimu kwa
maendeleo ya Taifa hasa katika mchango wake wa kupeleka maji katika mradi wa
bwawa la kufua umeme la Julius Nyerere linalojengwa katika Wilaya ya Rufiji
mkoani Pwani.
Ndolo ni bwawa ambalo linaungana na
mabwawa mengine makubwa yaNgapemba na Mende kumwaga maji yake katika Mto Mnyela
na Mburi.
Mkusanyiko wa maji hayo huchangia
asilimia 65 katika bwawa la Julius Nyerere.
Kamanda wa Uhifadhi Pori la Akiba la
Kilombero “A”, Bedui Mboto anasema TAWA imefanya kazi kurejesha uoto wa asili
katika pori hilo ambao uliharibiwa na shughuli za kibinadamu.
Pia wanaendelea kutoa elimu kwa
jamii kuhusiana na umuhimu wa kulinda na kuhifadhi mazingira hususani katika
pori hilo sambamba na kuhamasishawananchi kuwa na miradi rafiki kwa uhifadhi.
Hatua zaidi kulinda Pori la Akiba la Kilombero
Kamanda wa Uhifadhi TAWA Wilaya ya Kilombero, Bigilamungu Kagoma anasema kwa sasa ulinzi wa pori hilo umeimarishwa na kwamba vitendo vya uharifu ikiwemo ujangili na uvuvi haramu vimepungua.
Kagoma anasema wanatumia boti maalum
za doria katika mabwawa, kamera za kuchukua picha bila rubani (drone) pamoja na
askari wanaozunguka katika pori hilo usiku na mchana wakiwa na silaha za moto .
Mbali na kuimarisha ulinzi lakini
TAWA Kilombero tayari wameanza utaratibu wa kuweka vigingi katika maeneo ya
mipaka ya pori hilo ili kuzuia uvamizi ya makazi na shughuli za kilimo.
Mpaka kufikia Novemba 2023, tayari
wameweka vigingi 287 kati ya vigingi 389 wanavyolenga kuweka awamu ya kwanza.
Kagoma anasema wanatarajia kuongeza watumishi
kutoka 27 mpaka 82 pamoja na vitendea kazi mbalimbali, kama vile boti huku
akisema wamejipanga vizuri katika kufanya doria muda wote katika pori hilo.
Kwa mujibu wa TAWA Kilombero, katika
kipindi cha Julai hadi Novemba 2023, watuhumiwa 188 walikamatwa katika pori
hilo kwa makosa mbalimbali ikiwa ni pamoja na ulishaji wa mifugo hifadhini,
kilimo, uvuvi haramu na ukataji wa miti kwa matumizi mbalimbali.
Watuhumiwa hao walikamatwa baada ya
kukiuka Sheria ya Uhifadhi namba 5 ya mwaka 2009, huku ng’ombe 5,109,
nyavu/kokoro 35, majembe ya kukokotwa na ng'ombe 16 na matrekta matano navyo
vikikamatwa.
Comments
Post a Comment