WANANCHI 183,519 KUONDOKANA NA ADHA YA UKOSEFU WA MAJI KIBAHA BAADA YA MIRADI MITATU MIKUBWA YA KIMKAKATI KUANZA KUTEKELEZWA







Julieth Ngarabali , Kibaha  PWANI.

 

Wananchi  takribani 183,519  waliokuwa wakikabiliwa na adha ya ukosefu wa huduma ya maji safi  kwa zaidi ya miaka 20 sasa wanatarajia kuachana na adha hiyo baada ya Serikali  kutia  saini  na kukabidhi eneo lla utekelezaji wa miradi mitatu  ya kimkakati ya usambazaji maji  yenye thamani ya zaidi ya sh.48 Bilioni huko Kibaha Mkoani Pwani.

 

 

Picha za matukio  mbalimbali za utiaji saini    utekelezaji wa miradi mitatu  ya kimkakati ya usambazaji maji  yenye thamani ya zaidi ya sh.48 Bilioni huko Kibaha Mkoani Pwani baina  ya mamlaka ya maji safi na usafi wa mazingira Dar esalaam  (DAWASA) n.a  kandarasi  wawili  China Civil Communication and Engineering Company ((CCCEC ) na  Shanxi Construction Engineering Corporation and  Mineral Company (SCECMC)  .  


Utiaji saini  huo umefanyika katika viwanja  vya  Sekondari Pangani mjini Kibaha baina ya mamlaka ya maji safi na usafi wa mazingira Dar esalaam  (DAWASA) na  kampuni mbili za ujenzi  China Civil Communication and Engineering Company ((CCCEC ) na  Shanxi Construction Engineering Corporation and  Mineral Company (SCECMC)  na kushuhudiwa na  Waziri wa maji  Jumaa Aweso  na Viongozi wengine Mkoani Pwani .


Waziri  wa maji  Jumaa Aweso, mkuu wa Mkoa wa Pwani Abubakari Kunenge , Mbunge Kibaha Mjini Silvestry Koka  ni miongoni mwa walioshuhudia utiaji saini mkataba wa utekelezaji wa miradi mitatu mikubwa ya kimkakati ya usambazaji maji Mkoani Pwani. 


Wakizungumza  mara baada ya hafla hiyo, baadhi ya wananchi  wa Kata ya Pangani Mjini Kibaha wamesema  kwa zaidi ya miaka 20 wamekuwa wakipata kero ya ukosefu wa maji safi jambo ambalo limekuwa likiwathiri kiuchumi ,kijamii na  kiafya

 

"Tumekuwa tukitumia  maji ya madimbwi na mabwawa yasiyo salama na kusababisha homa za matumbo  apa maji ya rangi ya tope kabisa hivyo mradi huu ukikamilika utaleta faraja kwetu   na pia wanafunzi watawahi masomo maana hawataamka saa tisa usiku tena "amesema Augostino Mdachi

 

Mdachi amesema asilimia kubwa ya wananchi walikuwa wanafuata maji umbali wa zaidi ya km sita hivyo kuathiri hata shughuli zao za Kila siku za  kiuchumi.

 

Naye Asha Shabani amesema ukosefu wa huduma ya maji kutoka kwenye chanzo cha kuaminika imesababisha migogoro ya ndoa kwani baadhi yao wamekuwa wakiamka usiku kutafuta maji jambo ambalo lilikuwa likitafsiriwa na waume zao wanatumia mwanya huo kukutana na michepuko

 

Mmoja wa wanafunzi wa shule ya Pangani Mariam Saidi ameshukuru kusainiwa kwa miradi hiyo mikubwa kwani athari alizokuwa akizipata ni pamoja na kushindwa kuhudhuria masomo pindi anapokuwa kwenye hedhi  kutokana na changamoto hiyo ya maji.

 

Awali kaimu Afisa Mtendaji Mkuu wa DAWASA  Kiula Kingu akitoa taarifa ya utekelezaji miradi hiyo ameitaja ni mradi wa maji ya kimkakati Kwala wenye thamani ya sh. 23.6 Bilion ambao utahudumia watu 7,901  wa maeneo ya Kwala na vitongoji vyake ,bandari kavu  pamoja na viwanda vikubwa na vidogo 200.

 

Mhandisi Kingu ametaja mradi mwingine ni  wa Pangani unaotarajiwa kuhudumia watu zaidi ya  46,000  wa  Kata ya Pangani na baadhi ya majirani zao  wa kata ya Tangini mjini Kibaha na una thamani ya sh. 8.9 Bilioni na wa tatu ni mradi wa Kimbiji mpaka chuo cha uhasibu ( TIA) utakaonufaisha  watu 160,750  wa maeneo ya TAZARA,Ukonga hadi Gongola Mboto na utagharimu sh. 12.6  .

 

"Miradi hii yote itakamilika mwaka 2025  na itatekelezwa kwa fedha kutoka Serikali kuu chini ya usimamizi  wa wahandisi wa ndani na utekelezaji wa miradi hii yote mitatu utasaidia kumaliza changamoto ya upatikanaji wa huduma ya Maji Mkoani Pwani." amesema   Kiula

 

Mbunge jimbo la Kibaha Mjini Mh. Silvestry Koka ameomba utekelezaji wa miradi hiyo ukamilike kwa wakati ili Wananchi na wagonjwa wanaopata huduma  katika hospital ya rufaa ya Mkoa Pwani Tumbi hasa wajawazito  na wa upasuaji waweze kuwa na uhakika wa huduma hiyo.

 


" Kibaha ina kata  14 kati yake mbili  za Pangani na Viziwaziwa ndio zilikua na changamoto kubwa ya maji muda mrefu na kwamba sasa ujio wa mradi hii itabakia kata Moja ya Viziwaziwa ndio haina maji na kuomba wananchi wa eneo hilo nao wasogezewe " amesema Koka

 

Aidha Mkuu wa Mkoa wa Pwani  Mh. Abubakari Kunenge akitoa salamu amesema  kwa sasa upatikanaji wa huduma za maji ni asilimia   86  kwa mujibu wa takwimu kutoka DAWASA na RUWASA  na kwamba lengo ni kufikia asilimia 95 ifikapo mwaka 2025

 


"Sisi wakazi wa mikoa ya Dar esalaam na Pwani  tunasema maji ni sehemu ya huduma ya kijamii lakini pia ni nyenzo ya kiuchumi hasa Pwani ni Mkoa wa uwekezaji hivyo miradi hiyo mitatu ni muhimu sana mkono hapa"  amesema Kunenge

 

Kunenge ameongeza kuwa  Serikali inawekeza fedha nyingi  kwenye miradi hiyo na hivyo  kuomba wananchi wahakikishe miundombinu ya  miradi ya maji inatunzwa vizuri na  ankara za maji zilipwe vema.

 

Mara baada ya kushuhudia utiaji saini  na.makabidhiano ya eneo la ujenzi ,   Waziri mwenye dhamana  Mh. Jumaa Aweso amemuelekeza  kaimu Afisa Mtendaji Mkuu DAWASA Kingu kupeleka mradi wa maji kata ya Viziwaziwa Kibaha eneo ambalo halina kabisa huduma hiyo  na  kutaka ifikapo Februari mwaka 2024 maji yawe yanatoka  kwa wananchi eneo hilo

 


Aweso  pia ameihakikishia chama cha .Mapinduzi CCM kuwa atafanya kazi usiku na mchana kuhakikisha maji yanapatikana na pia yale yote walioahidi kwenye Ilani ya chama hicho ifikapo 2025 inakamilika na chama hicho kitaenda kupata ushindi wa kishindo.

 

"Nakuagiza mtendaji wetu wa DAWASA huu mradi wa Pangani  bora wafanye kazi kwa wakati  na  miradi hii ikikamilika wananchi wa Pwani wakitaka kuunganishiwa maji wasiletewe  mizengwe waunganishiwe  lakini na wao  wanawajibu wa kulipia ankara  ili miradi iwe endelevu" amesema Aweso

 

" Haiwezekani suala la manunguniko ya watu kulalamikia kubambikiziwa bili kila wakati  itushinde na hivyo sasa tunakwenda kufunga  luku kwenye huduma za maji. tukiamini  itaondoa hii kero hii " amesema 

 

Mwisho



Club News Editor

Comments

Popular posts from this blog

RC PWANI AONGOZA WAKAZI PWANI KUJIANDIKISHA KWENYE DAFTARI LA WAPIGA KURA

BARAZA LA MADIWANI KIBAHA MJINI LAMPONGEZA MKURUGENZI WAKE KWA KAZI NZURI ANAYOIFANYA SAMBAMBA NA KUONGEZA MAPATO.

RAIS SAMIA ATANGAZA KIBAHA MJINI KUWA MANISAPAA,MBUNGE KOKA AFURAHIA ASEMA KIBAHA ITANG'AA