KIBAHA YAZINDUA PROGRAM YA MALEZI, MAKUZI NA MAENDELEO YA AWALI YA MTOTO


 Julieth Ngarabali,   Kibaha

Halmashauri ya Wilaya ya Kibaha imezindua program Jumuishi ya Taifa ya malezi ,makuzi na maendeleo ya awali ya Mtoto ( PJT MMMAM) kwa lengo la kukabiliana na tatizo la udumavu, kuwapa huduma bora za malezi ya awali na programu za elimu ambazo zitawawezesha  watoto wenye umri wa miaka 0 hadi 8 kukua na kufikia ukuaji timilifu na hatimaye kuwa watu wazima wenye uwezo wa kufanya kazi za uzalishaji mali kwa tija hivyo kuchangia ukuaji wa uchumi wa Tanzania pamoja na kujenga jamii yenye amani na utulivu.

 Uzinduzi huo umefanyika kwa kushirikisha wadau mbalimbali ikiwemo taasisi ya Anjita Child Development Foundation,viongozi wa dini, kisiasa,sekta binafsi, wataalam mbali mbali na wamiliki wa vituo vya kulelea watoto wadogo katika halmashauri hiyo.


Program hii inaongozwa na kauli mbiu,"mtoto kwanza na watoto wetu tunu yetu""

Akizungumza kwenye uzinduzi huo kaimu Mkurugenzi halmashauri ya Kibaha ,Fatuma Kisalazo amesema programu hiyo pia itasaidia kumkuza mtoto kimwili ,kiakili, lugha, kijamii, kiutamaduni, kihisia na kimaadili.

Kisalazo amewaeleza wadau hao kuwa programu hiyo inalenga kutoa huduma za afya , lishe, malezi yenye mwitikio, ujifunzaji wa awali na ulinzi na usalama wa watoto wenye umri wa miaka 0 -8 na kuimarisha ushirikiano wa wadau wa sekta mbalimbali katika huduma za program hiyo.

 “naikumbusha jamii kuwa jukumu la kulea watoto na kuwalinda ni la jamii nzima wazazi walezi, serikali na wadau wote kila mmoja katika eneo lake ana wajibu wa kumlinda mtoto na kadhia za aina zote’’ amesema Kisalazo.

Ikumbukwe kwamba Program hii pia itasaidia kuboresha uratibu wa huduma kwa kuimarisha utekelezaji wa sheria na sera zinazohusu masuala ya MMMAM ikiwa ni pamoja na sheria ya Mtoto ya mwaka 2008, Sera ya Elimu na mafunzo ya mwaka 2014, sera ya afya ya mwaka 2007 ili kushughulikiwa kikamilifu mahitaji yote ya maendeleo ya watoto wenye umri wa miaka 0-8.

 Afisa ustawi wa jamii ,Yahya Mbogolume amewataka wazazi kutimiza majukum yao ya kimalezi sambamba na kushiriana na walimu kufuatilia maendeleo ya watoto wanapokua mashuleni.

Wadau walioshiriki uzinduzi huo wamesema programu hiyo ni nzuri ikitekelezwa kwa ufasaha kwani itasaidia taifa kuwa na viongozi wenye utilimifu na kuishauri serikali kukaa na wamiliki wa vituo na kuzungumza  nao kwani wanamengi kutoka kwa watoto wanaowalea lakini wanashindwa kuyatoa  kwa kutokua na ushahidi wa kutosha.

Mmoja wa wadau Deodan Katie amesema watoto wengi wanaharibika kutokana na vipindi vilivyo kwenye runinga havina maadili kwa watoto na kundi hilo lipewe elimu ya kujielewa na wajengewe kujiamini ili wanapokutana na changamoto waweze kuripoti.

Baadhi ya wadau wa Program Jumuishi ya Taifa ya malezi,makuzi na maendeleo ya awali ya mtoto  -PJT MMMAM wakifatilia mada mbalimbali kuhusiana na mpango huo zilizokuwa zikitolewa kwenye uzinduzi wa program hiyo wilayani Kibaha.

Awali Mkurugenzi wa Taasisi ya Anjita Child Development Foundation amesisitiza wadau kufanya kazi kwa kushirikiana, kutoa taarifa za utekelezaji na kuhimiza wadau na serikali katika kutenga bajeti za shughuli za malezi ,makuzi na maendeleo ya mtoto. 

Kwa mujibu wa Takwimu za Taifa za makisio ya idadi ya watu zilizotolewa na Idara ya Takwimu Taifa, Tanzania ina takriban watoto 16,524,201 (wavulana 8,328,142 na wasichana 8,196,056 ) wenye umri wa miaka 0-8 (ambao asilimia 30 ya watu wote) 

 Hii inamaanisha kuwa katika kila watu watatu,kuna mtoto mwenye umri wa miaka 0 mpaka nane na kwamba kundi hili linahitaji kuangaliwa kwa karibu na kufanyiwa uwekezaji ili waweze kuwa rasilimali bora yenye tija kwa familia na Taifa.

 

Baadhi ya wadau wa Program Jumuishi ya Taifa ya malezi,makuzi na maendeleo ya awali ya mtoto  -PJT MMMAM wakiwa kwenye picha ya pamoja mara baada ya uzinduzi wa program hiyo katika wilaya ya Kibaha Mkoani Pwani.


Club News Editor,  Julieth Ngarabali

Comments

Popular posts from this blog

RC PWANI AONGOZA WAKAZI PWANI KUJIANDIKISHA KWENYE DAFTARI LA WAPIGA KURA

BARAZA LA MADIWANI KIBAHA MJINI LAMPONGEZA MKURUGENZI WAKE KWA KAZI NZURI ANAYOIFANYA SAMBAMBA NA KUONGEZA MAPATO.

RAIS SAMIA ATANGAZA KIBAHA MJINI KUWA MANISAPAA,MBUNGE KOKA AFURAHIA ASEMA KIBAHA ITANG'AA