ANUSURIKA KUUAWA MARA TATU PORI LA AKIBA KILOMBERO.




 Ally Libenanga aliyewahi kunusurika kuuawa mara tatu na mamba na viboko wakati akivua samaki katika bwawa la Ndolo 


Na Gustaph Haule, Kilombero

ILIKUWA Novemba 23 Saa 10:30 jioni naingia katika kambi ya wavuvi ya Isherero katika Kijiji cha Idui kilichopo jirani na pori la akiba la Kilombero lililopo katika Halmashauri ya Wilaya ya Mlimba Mkoani Morogoro. 

Safari hiyo ya saa ,9 iliyoanzia katika eneo la Mikumi hadi katika Kijiji hicho ilinikutanisha na Ally Athumani Libenanga (43) aliyewahi kuwa mvuvi haramu katika bwawa la Ndolo lililopo katika pori hilo. 

Libenanga, baba wa watoto wanne kwa sasa ameachana na shughuli ya uvuvi haramu baada ya kukumbwa na mikasa mbalimbali ikiwemo kushambuliwa na Kiboko na Mamba ambayo imekuwa ikitishia uhai wake.

“Uvuvi haramu ni sumu,” anasema Libenanga akiwa nje ya nyumba yake ya chumba kimoja iliyojengwa kwa kutumia miti na udongo na kisha kuezekwa na nyasi .


Pichani baadhi ya nyumba za Wavuvi katika kambi ya Isherero iliyopo jirani na pori la akiba la Kilombero

Sababu kubwa iliyochangia Libenanga ambaye ni mzaliwa wa Wilaya ya Mahenge  mkoani Morogoro kuacha uvuvi haramu ni baada ya Serikali kuwaondoa watu wote waliovamia pori hilo wakiwemo wavuvi waliokuwa wakiendesha shughuli zao kinyume cha Sheria ya Uhifadhi namba 5 ya mwaka 2009.

Hatua hiyo ilikuja baada ya Serikali kulipandisha hadhi pori tengefu la Kilombero na kuwa pori la akiba la Kilombero Februari 2023 ambalo kwa sasa limegawanywa katika sehemu kuu mbili yaani pori la akiba Kilombero “A” na pori la akiba Kilombero “B”. 

Lengo la kupandisha hadhi pori hilo lilikuwa ni kuokoa viumbe pori wakiwemo wanyamapori ambao walikuwa hatarini kutoweka kutokana na shughuli za kibinadamu. 

Shughuli hizo ni pamoja na uvuvi haramu wa samaki, ukataji wa miti kwa ajili ya kuni, mkaa, kilimo, makazi ya watu, malisho ya mifugo na uwindaji haramu wa wanyamapori.

    Chati inayoonyesha mapori ya akiba ya wanyamapori matano ambayo ni makubwa zaidi Tanzania

Pori la Akiba la Kilombero ambalo liko chini ya Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania (TAWA) lina mabwawa makuu matatu; Ndolo, Ngapemba na Mende ambayo humwaga maji yake katika mito ya Mnyela na Mburi ambayo ni makazi ya viumbe mbalimbali wakiwemo samaki, mamba, viboko na nyoka. 

Hata hivyo, upekee wa bwawa la Ndolo ni makazi ya samaki aina ya vitoga, kambale, perege na “tigerfish” ambaye ni maarufu duniani. 

Umuhimu wa mito na mabwawa yaliyopo katika pori hilo ni mkubwa kwa sababu huchangia asilimia 65 ya maji katika mradi wa bwawa la kufua umeme la Mwalimu Nyerere lililopo Rufiji mkoani Pwani.

“Hifadhi ya pori la akiba Kilombero ina umuhimu wake kwa Taifa kwani mabwawa na mito hiyo ikikauka ni wazi kuwa bwawa la kufua umeme la Mwalimu Nyerere nalo litakufa,” anasema Kamanda wa Uhifadhi TAWA Wilaya ya Kilombero Bigilamungu Kagoma. 

Takwimu za Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyama Pori Tanzania ( TAWA) Kilombero zinaeleza kuwa kuanzia Julai hadi Novemba 2023, jumla ya watuhumiwa 188 walikamatwa kwa makosa mbalimbali ya ulishaji wa mifugo hifadhini, kilimo, uvuvi haramu na ukataji wa miti kwa matumizi mbalimbali.

Miongoni mwa vielelezo viliyokamatwa ni ng'ombe 5,109, nyavu/kokoro (35), majembe ya kukokotwa na ng'ombe (16) na matrekta matano na mitumbwi mbalimbali ya magome ya miti.

Chungu ya uvuvi haramu:

Libenanga ambaye kwa sasa anajishughulisha na kilimo anaweka bayana kuwa athari za uvuvi haramu ni kubwa kwani wakati wowote unaweza kupoteza maisha, kupata ulemavu, kupotelea gerezani na hatimaye kuacha familia ikiteseka.

Hatamani tena kufanya shughuli za uvuvi haramu kwa sababu iliyaweka maisha yake rehani zaidi ya mara tatu kwa kuvamiwa na mamba na viboko wakati akivua samaki katika bwawa la Ndolo kwa nyakati tofauti.

Mwaka 2017 akiwa katika mtumbwi katikati ya bwawa hilo alijikuta amedakwa na mamba katika mguu wake wa kulia na hivyo kujeruhiwa vibaya.

"Nilipambana na mamba kwa kumchoma na fimbo yenye ncha kali mdomoni mpaka akaniachia lakini kiukweli hali yangu ilikuwa mbaya kwani aliniachia majeraha ambayo niliyauguza wa muda mrefu,” anasema Libenanga huku akionyesha sehemu ya mguu wake aliyojeruhiwa.

Haikuishia hapo, siku moja mwaka 2019 wakati anaendelea na shughuli zake za uvuvi ghafla akang'atwa na mamba katika mkono wake wa kushoto na katika purukushani akajikuta amechanwa sehemu ya kidole gumba.

Mwaka 2020 akiwa anavua samaki kwa kutumia ndoano ya mkono katika bwawa hilo alijikuta anarukiwa na mamba lakini hakuweza kuguswa kwa kuwa alikimbia, Maisha ya uvuvi haramu kwa Libenanga hayakuwa rahisi. mwaka 2022,  akiwa na mwenzake katikati ya bwawa hilo walivamiwa na kiboko na mtumbwi wao wa mbao ulipinduliwa na mnyama huyo.

Baada ya kupinduka wote walifanikiwa kuogelea mpaka ufukwemi lakini hakuna yeyote aliyepata madhara zaidi ya kupoteza mtumbwi wao, siku hii haikuwa nzuri kwa Libenanga kwasababu ya hofu aliyokuwa nayo ya kupoteza uhai. 

    Pichani Kiboko wakiwa majini

Ilikuwa ni vita ya kufa au kupona

Ukiachia mbali misukosuko aliyokuwa anaipata ya kuvamiwa na wanyamapori lakini hatari zaidi ilikuwa ni mapigano kati ya wavuvi na wafugaji ambapo kila kundi likitaka kutumia bwawa hilo ambalo walilifanya kama kitega uchumi chao. 

"Sisi wavuvi ili tupate samaki lazima bwawa liwe na maji lakini wenzetu walikuwa wanaleta mifugo mingi kunywesha maji, jambo ambalo lilikuwa likisababisha maji kupungua na hivyo kushindwa kuingiza mitumbwi kwa shughuli ya uvuvi," anasema na kuongeza.

"Aisee! kuna siku nilipigwa na wafugaji hapa bwawani sitoweza kusahau nilitoka mbio kuwaita wenzangu lakini tulishindwa kwa kuwa wenzetu walikuwa na silaha zikiwemo fimbo, visu na mapanga lakini wote tulikuwa wavamizi tu.”

Mwanzo mpya wa uvuvi unaofuata sheria:

Baada ya udhibiti wa pori la akiba la Kilombero kuimarishwa, kwa sasa uvuvi haramu umekomeshwa kufuatia Serikali kuweka utaratibu wa watu kuvua samaki katika bwawa la Ndolo kwa vibali maalum. 

Wakati Libenanga akisifia utaratibu wa kukata vibali vya uvuvi katika bwawa hilo wapo baadhi ya wafanyabiashara wanaoishi katika kambi ya wavuvi ya Isherero wanasema shughuli za uvuvi zimesimama kwa muda, jambo ambalo linaathiri biashara zao. 

Mmoja wa wafanyabiashara hao, Amina Mohamed anasema umepita muda wa miezi miwili yupo kambini hapo lakini hakuna anachozalisha.

Biashara ya Amina katika kambi hiyo ni kuuza chipsi, bia na nguo aina zote. Kabla ya wavuvi kuzuiliwa kuingia bwawani hapo bila kibali, kipato chake kilikuwa Sh.30,000 mpaka Sh.50,000 kwa siku. 

"Nilikuja hapa nikanunua kipande cha ardhi nikaanza kujenga kibanda changu lakini toka nimejenga sijafanya chochote kwa kuwa sina hela maana nilikuwa nawategemea wavuvi wavue samaki wauze ndipo na mimi nifanye biashara lakini kwa sasa nipo nipo tu labda mpaka uvuvi rasmi utakapoanza,” anasema Amina. 

Sera ya Wanyamapori ya Tanzania ya mwaka 2007 inasisitiza kuwa Serikali na wadau wa uhifadhi kulinda shoroba za wanyama, njia za uhamaji, maeneo ya usalama wa wanyama, na kuhakikisha kwamba jamii zilizopo katika maeneo hayo ya wanyama zinafaidika vilivyo kutokana na uhifadhi wanyamapori.

Pia sera hiyo inaagiza kuzuia matumizi haramu ya wanyamapori nchini kote kwakuchukua hatua endelevu za usimamizi, ulinzi na kutekeleza sheria.

Afisa ujirani mwema wa pori la akiba Kilombero na mtaalam wa masuala ya uvuvi, Rehema Kaminyoge anasema tangu pori hilo lipandishwe hadhi mwaka huu, utaratibu wa uvuvi nao umebadilishwa. 

Miongoni mwa mambo ambayo yameongezeka ni kuweka ulinzi mkali wakati wa usiku na mchana kwa ajili ya kudhibiti uvuvi haramu uliokuwa ukifanyika hapo awali.

 
Afisa ujirani mwema wa pori la akiba Kilombero na mtaalam wa masuala ya uvuvi, Rehema Kaminyoge (Katikati) akielezea umuhimu wa bwawa la Ndolo kwa waandishi wa habari waliotembelea eneo hilo

  "Kwa sasa umewekwa utaratibu maalum wa mtu kuvua samaki katika bwawa hili na yule ambaye atashindwa kufuata utaratibu haruhusiwi kuvua samaki hapa na akikutwa askari watamkamata," anasema Rehema wakati nilipofanya naye mahojiano baada ya mafunzo ya kuripoti habari za bioanuai yaliyoandaliwa na kampuni ya Nukta Africa chini ya mradi wa USAID Tuhifadhi Maliasili. 

Kwa mujibu wa utaratibu huo, kila mvuvi anatakiwa kukata kibali ambacho atalipia kila siku Sh.5,000  na kibali hicho kitatumika siku moja tu anayotaka kuvua samaki. Kwa mchuuzi anapaswa kulipa Sh.4,000 kwa siku.

Rehema anasema kama mvuvi anataka kuvua samaki ndani ya miezi sita bila kupumzika anapaswa kulipia Sh.15,000 lakini kila siku atalipia Sh.2,000 kama gharama ya uendeshaji ambayo itatumika kuhifadhi na kuboresha mazingira ya bwawa Ndolo.

Utaratibu wa sasa ni mvuvi kukata kibali cha miezi sita, kibali cha siku moja, kibali cha wachuuzi na vibali vya vyombo kama vile mitumbwi.

"Kasi ya wavuvi hao kukata vibali bado ni ndogo kwani mpaka Novemba 30 mwaka huu walikuwa wamekata vibali wavuvi nane licha ya kupeleka wataalamu wa kuwasaidia kukata vibali hivyo kambini hapo,"amesema Rehema.

Rehema ,kutokana na hali hiyo TAWA itaendelea kutoa elimu na kuhamasisha wavuvi kuona umuhimu wa kukata vibali hivyo lakini pia wataendelea na mpango wa kupeleka wataalamu kambini hapo ili kuwarahisishia ukataji wa vibali hivyo.

Elimu ya uhifadhi nayo muhimu:

Kamanda wa Uhifadhi pori la akiba Kilombero "A" Adam Mboto, anasema kazi kubwa waliyoifanya ni kuhakikisha wanawahamisha wananchi ndani ya pori hilo na kuwapa maeneo umbali wa mita 500 kutoka hifadhini.

Pia TAWA inatoa elimu kwa wananchi wa vijiji vinavyozunguka pori hilo kuhusu umuhimu wa kuhifadhi mazingira na kuepuka vitendo vyovyote vilivyo kinyume na uhifadhi. 

Kuhusu uvuvi uliokuwa ukiendelea katika pori hilo, Mboto anasema mwaka 2020 walianza kuweka utaratibu maalum wa kulinda hifadhi hiyo ambapo miongoni mwa taratibu hizo ziligusa masuala ya uvuvi wa ujirani mwema.

"Kwasasa tunasimamia sheria ya uhifadhi namba 5 ya mwaka 2009 na taratibu za uvuvi zilizowekwa na mvuvi ambaye anashindwa kuwa na kibali akajitokeza na kuanza kuvua samaki katika bwawa hili hatoachwa salama kwani sheria itafuata mkondo kwa kuchukua hatua stahiki," Mboto anafafanua wakati wa mafunzo kwa vitendo kuhusu kuripoti habari za bioanuai yaliyoandaliwa na kampuni ya Nukta Africa chini ya ufadhili wa mradi wa USAID Tuhifadhi Maliasili. 

Sheria ya Uhifadhi ya Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania (TAWA) namba 5 ya mwaka 2009 inaeleza kuwa mtu yeyote anayekutwa katika hifadhi akifanya shughuli yoyote ya kibinadamu akikamatwa atakuwa amefanya kosa la jinai.

Kamanda wa uhifadhi TAWA Wilaya ya Kilombero Bigilamungu Kagoma anasema  kwasasa wamejipanga kikamilifu kudhibiti ujangili na uharibifu wa mazingira katika pori hilo.

Anasema askari maalum wanalinda hifadhi hiyo usiku na mchana kwa kutumia silaha za moto pamoja na kutumia teknolojia ya ndege zisizo na rubani (drone) kufuatilia usalama wa pori hilo.

Kamanda wa Uhifadhi Pori la Akiba Kilombero "A''Adam Mboto akitoa elimu kwa wavuvi waliopo Kambi ya Isherero juu ya umuhimu wa kukata kibali cha uvuvi katika bwawa lililopo ndani ya Hifadhi hiyo.picha na Gustafu Haule 



Club News Editor - Julieth Ngarabali

Comments

Popular posts from this blog

RC PWANI AONGOZA WAKAZI PWANI KUJIANDIKISHA KWENYE DAFTARI LA WAPIGA KURA

BARAZA LA MADIWANI KIBAHA MJINI LAMPONGEZA MKURUGENZI WAKE KWA KAZI NZURI ANAYOIFANYA SAMBAMBA NA KUONGEZA MAPATO.

RAIS SAMIA ATANGAZA KIBAHA MJINI KUWA MANISAPAA,MBUNGE KOKA AFURAHIA ASEMA KIBAHA ITANG'AA